Kamati ya Bunge ya UKIMWI na madawa ya kulevya ilikutana na Baraza la Taifa la Watu Wanaoishi na VVU (NACOPHA) jijini Dar es Salaam na kujadili mambo mbalimbali ikiwemo kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya Baraza na kamati hiyo kwa lengo la kuwasaidia watu wanaoishi na VVU kupata huduma bora za afya na kuishi maisha bora
Kamati ya Bunge ililipongeza baraza kwa kazi kubwa Zinazofanywa kupitia viongozi wake kutokana na mafanikio yalioainishwa, Pamoja na hayo kamati ya Bunge imeahidi kushughulikia changamoto zilizoanishwa na Baraza ikiwemo suala la kuhakikisha Baraza linapata ofisi ya kudumu, pamoja na Viongozi wa Konga kupatiwa ofisi katika kila Halmashauri.
Mbunge kutoka Nsimbo katavi Mheshimiwa Richard Mbogo ambae ni mjumbe wa kamati ya Bunge- alisema “ Sisi kama kamati ya Bunge tutakaa na Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI kupitia kamati za UKIMWI za Halmashauri na kuwashauri kuwapatia viongozi wa Konga ofisi katika kila Halmashauri, ili waweze kufanya kazi kwa ukaribu zaidi na Halmashauri katika mwitikio wa UKIMWI”.
Kuhusu ofisi ya makao makuu ya Baraza kamati hiyo iliahidi kukaa na shirika la Taifa la nyumba na kuona ni kwa namna gani wanaweza kulipatia Baraza sehemu kwa ajili ya ofisi ili kuliwezesha kufanya shughuli zake kwa ufanisi zaidi.
Kwa upande wake mjumbe wa kamati hiyo Mheshimiwa Nasari Yahaya Omari alilihakikishia Baraza kuwa kamati itatoa ushirikiano wa karibu pale unapohitajika ikiwemo katika kutatua  changamoto mbalimbali, pia aliahidi kukaa na Serikali pamoja na mifuko ya Bima ya afya na kutazama vikwazo vinavyopelekea kutopatikana kwa huduma za bima  ya afya kwa watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (WAVIU).
Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza Bwana Deogratius Rutatwa ameishukuru kamati ya Bunge kwa kujitolea kufikisha matakwa ya Baraza kwa TAMISEMI ikiwemo kuishauri kufanya kazi kwa ukaribu na Konga.
Aidha ameiomba kamati kuishauri TAMISEMI kutengeneza waraka utakaoonyesha Halmashauri inatakiwa kufanya kazi na WAVIU

Katika hatua nyingine Bwana Rutatwa alimefurahishwa na kitendo cha kamati hiyo kutoa fursa ya kuwatumia WAVIU katika shughuli za mwitikio wa UKIMWI na katika matamasha makubwa ili kuihamasisha jamii juu ya maswala ya UKIMWI