Na Friday Simbaya, IRINGA
Mkuu wa Wilaya ya Iringa Richard Kasesela, amewataka wanaume kujitokeza kwa wingi kupima VVU ili kujua hali zao na kama wakugundulika waanze dawa mara moja.
Alisema kuwa utafiti unaonesha kwamba wanaume wako nyuma katika masuala ya kupima VVU ukilinganisha na wanawake.
Kasesela alisema hayo wiki iliyopita wakati wa uzinduzi wa filamu itwayo ‘PILI’ ya masuala ya VVU na UKIMWI katika Mkoa wa Iringa katika viwanja vya Mwembetogwa, iliyoanza kuonekana kuanzia saa moja 1 jioni hadi saa tatu usiku.
Alisema kuwa Iringa inakabiliwa na changamoto ya masuala ya UKIMWI kwa vile inashika nafasi ya pili katika maambukizi ya VVU baada ya Mkoa wa Njombe anaoshika nafasi ya kwanza kitaifa.
Kasesela alieleza kuwa  kuna faida ya kupima VVU na hatimaye kujua hali yako kwa vile Serikali inatoa ARVs za kupunguza makali ya VVU bure kupitia Msaada wa Mfuko wa dharura wa Raisi wa Marekani wa kupambana na UKIMWI (PEPFAR).
“Kupima VVU na kujua hali zetu za afya hasa kwa wanaume kutapunguza kasi ya maambukizi ya VVU mkoani Iringa, hivyo naomba wanaume wenzangu tuwe mstari wa mbele” Alihimiza DC Kasesela.

Pia alilipongeza Baraza la Taifa la Watu Wanaishi na VVU (NACOPHA) kwa kushirikiana na Ubalozi wa Marekani kwa onesho la filamu ya “PILI”.
Inalenga kuwafikishia ujumbe vijanakukiwa ni mwendelezo wa maadhimisho ya miaka 15 ya msaada wa PEPFAR katika kuwezesha wanaoishi na VVU (WAVIU) hasa vijana.
 Mratibu wa uzinduzi wa filamu ya “PILI” kutoka NACOPHA bwana Edward Uisso alisema lengo kuu la onesho la filamu/sinema hii ni ukuza ongezeko na ufikiwaji wa huduma za VVU hususani kwenye tiba na matunzo miongoni mwa vijana wadogo wanaoishi na VVU kupitia kutambua mchango na msaada wa PEPFAR katika mwitikio wa kitaifa wa UKIMWI kwa kutumia WAVIU kama wanufaikaji wa msaada kutoka PEPFAR nchini Tanzania.

Aliongeza kuwa malengo mengine ni kushirikisha jamii katika ongezeko la ufikiwaji na utumiaji wa huduma za VVU hasa kwenye tiba na matunzo na kutumia filamu hii kama zana ya uwezeshi  kwa vijana wadogo wanaoishi na VVU katika kutatua na kupambana dhidi ya unyanyapaa na ubaguzi.
Uisso aliongeza kuwa unyanyapaa binafsi kwa WAVIU bado ni changamoto kubwa ukiachilia mbali unyanyapaa utokanao na tamaduni na imani za kidini.
Alisema ushirikishwaji wa jamii ni ufunguo katika kuelimisha jamii juu ya madhara ya unyanyapaa kwa WAVIU na katika kufikia sifuri ya unyanyapaa ifikapo mwaka 2030.
“Uzinduzi huu wa filamu ya PILI ni wa tano kimkoa,  kwani kwa mara ya kwanza filamu hii ilizinduliwa kwa mkoa wa DSM tarehe 8/11/2018, Mwanza tarehe 23/11/2018, Mbeya tarehe 30/11/2018, Njombe ni leo tarehe 7/12/2018 na kilele kitakuwa kwa Mkoa wa Iringa tarehe 14/12/2018 ikiwa ni kubadilishana uzoefu kwa watu wanaoishi na VVU kama wanufaikiaji wa msaada wa PEPFAR nchini”. Alisema Uisso.



PILI anaishi  kijijini nchini Tanzania, akifanya kazi ya kibarura shambani akilipwa ujira wa chini ya dola mbili (Sh 2,600) kwa siku ili aweze kupata chakula kwa watoto wake wawili
Anaishi anahangahika kukabiliana na hali yake ya kuwa na VVU kwa kificho.