Mwaka 2000 Tanzania ilitangaza UKIMWI kuwa janga la Kitaifa. Katika kuimarisha juhudi hizi, mwaka 2004,  serikali iliweka mpango wa upatikanaji bure wa dawa za kufubaza makali ya VVU na kuhamasisha upimaji wa VVU. Hadi sasa kwa mujibu wa takwimu zilizopo takribani watu 1,400,000 wanaishi na maambukizi ya VVU na kati ya hao, takribani watu 850,000 wanatumia dawa (UNAIDS 2017). Yote haya ni matokeo chanya ya juhudi za serikali ambazo zimechangia kupungua kwa maambukizi ya VVU  kutoka asilimia 8.3% (2003) hadi aslimia 5.3% (THIMS 2012). Hata hivyo, pamoja na juhudi hizi, maambukizi ya VVU yanaonekana kuongezeka kwa kasi katika kundi la vijana wa umri kati ya miaka 19 hadi 35 ukilinganisha na makundi mengine.

Katika hotuba yake Mheshimiwa. Rais Dr. John Joseph Pombe Magufuli  aliyoitoa kwenye kilele cha maadhimisho wiki ya vijana,kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Kuzima Mwenge wa Uhuru  tarehe 14th October, 2017 huko Zanzibar, kwa  kunukuu maneno yake mwenyewe alisema; Vijana ndio uhai na nguvu kazi ya taifa hili..; Taifa hili ni lenu..; Mjihadhari na tabia za matumizi ya madawa ya kulevya na kufanya ngono zembe...” Kauli hii ya Mkuu wa Nchi ni ya kupongezwa sana kwani inavunja ukimya ,kuamsha na kuhamashisha juhudi za Kitaifa zinazolenga  kufikia malengo ya 90-90-90 ifikapo 2020,  vijana wakipewa kipaumbele. Sisi Baraza la Taifa la Watu Wanaoishi na VVU (NACOPHA) tumefarijika sana na kauli hii ya Kiongozi wa Nchi kwa vijana.   Tunaipongeza sana.

Akimkaribisha Mheshimiwa Rais kuongea na wananchi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Jenista Mhagama alisema kuwa; mojawapo ya mafanikio ya mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2017 ni pamoja na kuhamashisha upimaji wa VVU kwa vijana. Katika mbio za Mwenge za mwaka huu takribani watu 80,000 walijitokeza kupima na kujua hali zao miongoni mwao wakiwemo vijana.

Kwa kupitia taarifa hii kwa vyombo vya habari NACOPHA tunaomba pongezi zetu za dhati zimfikie Mhe. Rais Dr. John Joseph Pombe Magufuli kwani ni  imani yetu NACOPHA kuwa kauli hii itaamsha upya ari na kuongeza kasi ya mwitikio kwa UKIMWI kwa Viongozi na  mamlaka zote za  Serikali, mashirika ya kijamii  , Wadau wa maendeleo , vyombo vya habari , viongozi wa dini, jamii kwa ujumla na hasa vijana.

Ni ukweli usiopingika kuwa, matumizi ya dawa za kulevya na ngono zembe ni vichocheo vikubwa vya maambukizi mapya ya VVU na hasa kwa vijana. Vijana wengi na hasa wa kike wapo katika hatari kubwa Zaidi ya kupata maambukizi ya VVU kutokana na tabia hizi. Hata  hivyo  kwa sasa ni vijana wachache sana wanaojitokeza kupima na  kujua hali zao za afya. Hii ni changamoto kubwa katika kufikia azma ya serikali kufikia malengo ya 90-90-90 ikiwa ni pamoja na kujua hali yao ya maambukizi ya VVU; kuanza tiba; na kufubaza makali ya VVU. Ombi letu  Baraza kwa Mheshimiw Rais  ni: 

·         Kuendelea kuhamashisha  juhudi za upimaji wa VVU ili kuhakikisha watu wote wanaoishi na maambukizi ya VVU  wanapima na kujua hali zao za afya, wale wote wanaopatikana wanaishi na Maambukizi wanaanza mara moja na kudumu kwenye tiba, na pia wote walio kwenye tiba wanafuasa tiba kwa usahihi ili  kufubaza makali ya VVU. 

·         Kusisitiza na kusimamia viongozi wote kwa ngazi zote kuendelea kuhimiza na kutoa adhari kwa wananchi wa makundi yote, kuepuka maabukizi ya UKIMWI kwani bado Upo  na  maabukizi yanaendelea. Lengo ni kutokomeza UKIMWI ifikapo 2030

·         Kutoa msukumo mpya na kuhuisha sera ya taifa ya UKIMWI ya 2001 ili iweze kuendana na mikakati na uhitaji wa mwitikio wa UKIMWI kwa sasa na hasa wakati huu  wa awamu ya Tano

·         Kuwawezesha WAVIU na hasa vijana kuwa na uhakika wa kupata dawa  kwa magonjwa nyemelezi kwani kwa sasa dawa hizi hazipatikani na ni muhimu kwa ufuasi sahihi wa dawa

·         Kuhamasisha jamii kuondokana na Unyapapaa kwa WAVIU kwani hiki ni kikwazo kikubwa kufikia malengo ya 90 90 90

Ni rai yetu kwa watanzania wote , kuwa ni wajibu  wetu sote , na hasa kwa  kila kijana kuitikia wito wa mheshimiwa rais kuhakikisha wanalinda afya zao kwa kuepuka na kujilinda na vishawishi na tabia hatarishi kupata maambukizi ya VVU. Wazazi , walezi, Viongozi wa dini na wadau wengine kwa nafasi zetu , kuumunga mkono Mheshimiwa rais na kuwa karibu na vijana katika kuwaongoza na kuwaelimisha juu ya tabia hatarishi na kuwasaidia kuepuka maambukizi ya UKIMWI na madhara mengine yatokanayo na Ngono zembe na matumizi ya madawa ya kulevya.

Kwenu  ninyi Vyombo vya habari, mnalo jukumu kubwa kwa jamii, hususani vijana kuhakisha mnatoa taaarifa za mara kwa mara  mkielimisha na kuhamsisha jamii kupata huduma mbali mbali za kudhibiti UKIMWI  na hasa juu ya afya ya uzazi kwa Vijana. Napenda kusisitiza kuwa UKIMWI bado upo.

Tunapenda kutumia fursa hii kuwashukuru wadau wote ikiwa ni pamoja na  Serikali yetu ,  Bunge la Jamuhuiri ya Muungano wa Tanzania, USAID ,UNAIDS Mfuko wa Dunia wa UKIMWI, TB na Malaria, Vyombo Vya habari   na wengine wote kwa kuliwezesha baraza kufanya kazi zake kwa ufanisi
Mwisho kabisa, Tunapenda kumhakikishia Mheshimiwa  Rais utayari wa  Baraza na watu wanaoishi na VVU kwa ujumla wetu katika juhudi za Serikali za kuimarisha afya za vijana ili washiriki kikamilifu kuijenga Tanzania ya uchumi wa  Viwanda.

ASANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA.

Justine Mwinuka
Mwenyekiti

Baraza la Taifa la Watu Wanaoishi na VVU (NACOPHA)