WATANZANIA WAISHIO NA VVU WAASWA KUENDELEA KUTUMIA DAWA ZA KUFUBAZA VIRUSI



NA.MWANDISHI WETU
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Uratibu na Uwekezaji, Dorothy Mwaluko amewaasa Watanzania wanaoishi na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi kuendelea kutumia dawa za kufubaza virusi hivyo ili waweze kuishi maisha yenye afya na amani wakati wote.

Ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wanachama wa Baraza la Watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI katika Konga ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero Mkoani alipowatembelea kukagua utekelezaji wa majukumu ikiwa ni pamoja na namna konga hiyo inavyoendesha shughuli za uzalishaji Wilayani hapo Oktoba 17, 2019 Mkoani Morogoro.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji) Bi. Dorothy Mwaluko akizungumza na wajumbe wa Baraza la watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI wa KONGO ya Wilaya ya Kilombero alipowatembelea kuangalia namna wanavyoendesha shughuli zao za kimaendeleo na kuwajulia hali tarehe 17 Oktoba, 2019.

"Kipekee ninawapongeza kwa ujasiri wenu wa kujitokeza na kuonesha ulimwengu kuwa janga hili lipo na ni letu sote, kwani naamini hakuna mtu ambaye halijamgusa kwa namna moja au nyingine hivyo niwaombe mjitahidi kuendelea kutumia dawa hizi za kufubaza makali ya virusi ili kuendelea kuimarika zaidi,"alisema Mwaluko.

Baadhi ya wanachama wa Baraza la Watu wanaoishi na VVU wa KONGA ya Kilombero awakifuatilia hotuba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji) Bi. Dorothy Mwaluko (hayupo pichani) wakati wa ziara yake katika ofisi za konga hiyo, Oktoba 17, 2019.
Aliwasisitiza kuendelea kuwa mabalozi wazuri kwa wengine ambao hawajatambua hali zao na wale waliotambua hali zao kuendelea kufubaza virusi na kutoacha kutumia  dawa hizo kwa kuzingatia umuhimu wake.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji) Bi. Dorothy Mwaluko akizungumza na umoja wa watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI wa KONGO ya Wilaya ya Kilombero alipowatembelea kuangalia namna tekeleza shughuli zao za kimaendeleo tarehe 17 Oktoba, 2019.

"Napenda kuwahamasisha msiache wala kuchoka kutumia dawa hizi kwa kuzingatia umuhimu wake katika kuhakikisha zinawapa nafuu na kuondoa magonjwa nyemelezi kuendelea kuwa na afya njema na kushiriki katika shughuli za kimaendeleo na kufanya dunia mahali salama pa kuishi,"alisisitiza Mwaluko.

Mwenyekiti wa Baraza la Watu wanaoishi na VVU wa Konga ya Kilombero, Halida Ally akisoma taarifa ya Konga hiyo kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji) Bi. Dorothy Mwaluko (hayupo pichani) wakati wa ziara yake katika konga hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utafiti na Tathimini kutoka Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Dkt. Jerome Kamwela aklieleza kuwa, hali ya kiwango cha maambukizi Mapya ni asilimia 4.7 Kitaifa na maambukizi hayo ni mengi kwa wanawake kuliko wanaume hivyo Serikali itaendeelea kuhudumia kundi hili kwa kuhakikisha lilapewa dawa hizo kwa kadri itakiwavyo.

Mkurugenzi wa Utafiti na Tathimini kutoka Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Dkt. Jerome Kamwela akizungumza jambo kuhusu hali ya Maambukizi mapya kwa wanakonga ya Wilaya ya Kilombero wakati wa ziara ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji) Bi. Dorothy Mwaluko.


"Serikali imejipanga kuhakikisha kundi la WAVIU wote wanahudumiwa na kupatiwa mahitaji yao muhimu ikiwemo upatikanaji wa dawa za kufubaza makali ya virusi (ARV) hivyo na kuhakikisha kundi kubwa la wanawake ambao ndiyo wanaoathiriwa zaidi linafikiwa kadiri iwezekanavyo na hii itaendeelea kusaidia kundi hilo kupunguza hatari ya kuingia katika maambukizi mapya,"alieleza Dkt.Kamwela.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji) Bi. Dorothy Mwaluko akiangalia  baadhi ya bidhaa zilizotengenezwa na wanachanama wa KONGA ya WAVIU iliyopo Kilombero wakati wa ziara yake katika konga hiyo tarehe 17 Oktoba, 2019.
Aliongezea kuwa takwimu zinaonesha hali ya maambukizi mapya kwa kila mwaka ni watu 72000 ambapo kundi la vijana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 24 linaongoza kwa asilimia 40 na kueleza kundi la wanawake wanachangia asilimia 80 ya maambukizi hayo.
"Serikali imetoa kipaumbele kuwa mwitikio wa masuala ya UKIMWI umelenga kundi la vijana ili kupunguza maambukizi mapya yanayolikumba kundi hilo,"alifafanua Dkt.Kamwela.
Aliongezea kuwa wananchi wasipotambua hali zao mapema wanasababisha kuanza tiba kwa kuchelewa na hivyo kulazimika kuanza dawa wakati wa hatari na kuwalazimu kuwa na juhudi za ziada katika kutumia dawa ili kutokomeza maambukizi mapya na kufubaza virusi vya UKIMWI.

Aidha Mwenyekiti wa Baraza la Watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi wa Konga hiyo Halida Ally alieleza kuwa hali ya utoro wa dawa imechangia kuongezeka kwa maambukizi mapya ambapo walifanikiwa kuhamasisha watu 30,712 kupima hali zao ambapo jumla ya watu 2,038 walikutwa na maambukizi kati yao wanawake ni 1,327  na wanaume ni 711.

Mwenyekiti wa Konga ya watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi wilayani ya Kirombero Halida Ally akimuonesha Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji) Bi. Dorothy Mwaluko bidhaa mbalimbali wanazotengeneza katika Konga yao ikiwa ni sehemu ya miradi inayowasaidia kujipatia kipato na kuinua uchumi wao alipotembelea konga hiyo Oktoba 17, 2019.
Alisema hali ya utoro wa dawa ni changamoto katika kuhudumia kundi hilo inayochangiwa na uwepo wa sababu mbalimbali ambapo katika kundi la WAVIU 2,038 wanaotumia dawa za kufubaza virusi ni 1,707 kati yao wanawake ni 1,034 na wanaume ni 673 katika kundi hilo watoro wa dawa ni 996 kati yao wanaume ni 335 na wanawake ni 673 hali ambayo inachangia kuongezeka kwa maambukizi mapya na kuongeza ukubwa wa janga hilo katika Halmashauri yao.

Naye mmoja ya wanachama wa konga hiyo Betina Januari aliipongeza Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali katika mapambano dhidi ya Ukimwi na kuahidi uendelea kutoa ushirikiano katika jitihada za kuwawekea mazingira wezeshi na kufikia malengo ya sufuri tatu ifikapo 2030.

KONGA Kilombero ni Baraza la Taifa la Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (VVU) ngazi ya Wilaya. KONGA ya Kilombero imeundwa mwaka 2013 ikiwa na vikundi 14 vyenye jumla ya wanachama 354 ambapo wanawake ni 237 na wanaume 117.

Mratibu UKIMWI mkoa wa Morogoro Bi. Ndayahunda Hendry akizungumza jambo wakati wa mkutano huo.

(PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU)

KONGA KINONDONI YAFANYA UCHAGUZI WA VIONGOZI 2019

Konga ya Baraza la Taifa la Watu waishio na Virusi vya UKIMWI Tanzania (NACOPHA) halmashauri  ya wilaya ya Kinondoni imefanya uchaguzi wa viongozi wa konga hiyo mapema tarehe 23 /2/2019 katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya kinondoni.

Uchaguzi ulifanyika kwa ufadhili wa watu wa Marekani (USAID) Kupitia Mradi wa CHSSP unaotekelezwa na JSI, ambao moja ya malengo yake ni kuzijengea uwezo Konga katika masuala ya uongozi bora.


Uchaguzi huo ulisimamiwa na Viongozi kutoka halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni, Mratibu wa NACOPHA Kanda ya Dar es Salaam, wenyeviti wa kamati ya kudhibiti UKIMWI (CMACs), Mwakilishi wa mratibu wa UKIMWI ngazi ya halmashauri (CHACs) Mwakilishi wa Mratibu wa UKIMWI wilaya upande wa tiba (DACC) pamoja na Mratibu wa Mradi wa CHSSP kutoka JSI.

Wageni waliohudhulia kushuhudia uchaguzi huo ni pamoja na baadhi ya viongozi kutoka Konga jirani ambazo ni  Temeke, Ilala, Kigamboni na Ubungo.
Viongozi waliochaguliwa katika uchaguzi huo ni pamoja na:
Mwenyekiti - Juma Galaba.                          
makamu-nikokwisa Jeremiah.
Katibu-Suleiman Lweno.
Mwekahazina-Kisa Mbonile.

Viongozi wengine waliochaguliwa ni wajumbe wa Konga, Uwakilishi wa Vijana, Me - Said hamis na Mansue Ramadhani.  Ke- Shan Ally na Catherin Swai , Wawakilishi wa Wazee me- Mtume Mmakasa na Shahaban Bwanga. Ke ni Aisha kupanga na Doto Sanga pamoja na wajumbe wawili watakao wakilisha katika kamati ya kudhibiti UKIMWI ya Wilaya (CMAC) ambao ni Majuto Mwinyihija na Margret   Sinda
 
Baraza kupitia Afisa Mtendaji Mkuu inatoa pongezi kwa viongozi waliochaguliwa na kuwataka watekeleze wajibu wao kufuatana na sheria ya baraza inavyowataka wafanye “Nawapongeza Sana. Viongozi wote karibuni kwenye ofisi yenu tujuane tupange kazi kwa pamoja, msihofu tuko tayari kwa uwajibikaji. Ahsante kwa uongozi uliopita kuwezesha hili pamoja na JSI na ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa pamoja na CHAC. Ahsante Mratibu wa Kanda ya Dar es Salaam kwa kutuwakilisha. Ahasante Viongozi wa Konga zingine kwa kuonyesha mshikamano. Tushikamane sote kwa maslahi na ustawi wa WAVIU wote Tanzania” shukrani za Afisa Mtendaji Mkuu.
 

Hivi sasa Baraza lina konga zipatazo 167. Baraza linatoa shukrani za dhati kwa JSI R&T kupitia mradi wa CHSSP kwa kufanya kazi kwa Karibu na Baraza kwa kuhakikisha malengo ya pamoja ya kufikia 90-90-90 yanafikiwa.

ZIARA YA MAFUNZO NA KUBADILISHANA UZOEFU WILAYANI MBOZI


Baraza la Taifa la Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI Tanzania (#NACOPHA) Kupitia ufadhili wa shirika la umoja wa mataifa la kupambana na UKIMWI (#UNAIDS) liliandaa ziara ya siku mbili ya kuongeza ujuzi kwa konga zake na halmashauri katika kuongeza hamasa ya upimaji na ufuasi wa dawa kwa kupitia mbinu ya kushirikishana uzoefu baina ya konga zake katika masuala mazima ya Usimamizi, uendeshaji, ustawi pamoja na faida ya uwepo wa vikundi wezeshi kwa Watu wanaoishi na VVU pamoja na Halmashauri kwa ujumla.


kutokana na hatua kubwa ambayo halmashauri ya Mbozi imepiga katika shughuli zake za muitikio wa UKIMWI kupitia ushirikishwaji wa konga pamoja na usimamizi mzuri wa vikundi vya wezeshi vya watu wanaoishi na VVU (Vikundi Wezeshi) Baraza lilichagua halmashauri hiyo kuwa wenyeji wa ziara hiyo ya siku mbili kwa wajumbe kutokea katika halmashauri nne za Songea Dc, Makete, Njombe Dc pamoja na Rungwe Dc kusafiri na kwenda kujifunza na kubadilishana uzoefu na halmashauri ya Mbozi katika masula mazima ya uhamasishaji upimaji na ufuasi mzuri wa dawa kupitia vikundi wezeshi vya WAVIU.

 
 Ziara hii ilijumuhisha viongozi wa konga, wenyeviti wa kamati ya kudhibiti UKIMWI (CMACs), waratibu wa UKIMWI ngazi ya halmashauri (CHACs), wawakilishi wa viongozi wa vikundi vya WAVIU kutokea katika halmashauri tajwa. Ziara hii ilikuwa yenye mafanikio makubwa kwani kupitia wenyeji ambao ni Mbozi waliweza kushirikisha konga alikwa zote na kujionea namna gani konga ya Mbozi imepiga hatua kubwa katika muitikio wa UKIMWI, maendeleo ya vikundi wezeshi pamoja na ufuasi mzuri wa dawa kwa WAVIU ndani ya halmashauri.


Wajumbe waliweza kutembelea mojawapo ya kituo cha tiba na matunzo (CTC) na kujifunza namna ya ushirikishwaji wa WAVIU kama watoa huduma ndani ya jamii ulivyoweza kupunguza changamoto ya utoro wa dawa na kuongeza hamasa ya upimaji kwa jamii, pia wajumbe waliweza kutembelea mojawapo ya kikundi wezeshi cha WAVIU kata ya ICHESA na kujionea namna ya mfano wa vikundi wezeshi unavyofanya kazi na kuleta mabadiliko chanya kwa WAVIU na halmashauri kwa ujumla. 


Mwisho wa ziara wajumbe wote kutokea halmashauri zote nne waliweza kutoa ushuhuda wao wa namna gani wamefurahia na kujifunza kupitia ziara hii kisha kuhaidi kwenda kufanyia kazi maeneo ambayo walibaini ni mapungufu yao ambayo yanasababisha kwa namna moja ama nyingine kutofika kiwango cha maendeleo kama halmashauri ya Mbozi walichokifikia na watafanya hivyo baada ya kurejea katika halmashauri zao.



Wenyeviti wa halmashauri pamoja na mkurugenzi wa halmashauri ya Mbozi walitoa shukrani zao kwa UNAIDS kupitia NACOPHA kwa kuwezesha ziara hii na kuomba pale inapowezekana kuendelea kuwezesha halmashauri zingine kuja kutembelea na kujifunza katika halmashauri ya Mbozi.

ZIARA YA MAFUNZO ILIVYOFANYIKA KATIKA KONGA YA MULEBA

Mnamo tarehe 5 na 6 Februari 2019 chini ya ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UNAIDS Ofisi ya NACOPHA Kanda ya Mwanza ilifanya ziara 
ya kimafunzo ya kubadilishana uzoefu juu ya utekeleaji wa shughuli za mwitikio wa
UKIMWI ili kuhakikisha kuwa 90% 90% 90%  zinafikiwa ifikapo 2030.  ( ambapo 90% ya kwanza ni kwa waliopima afya zao watambue hali zao za maambukizi, 90% ya pili ni wanaostahili kupatiwatiba wanapata tiba na kubakia katika tiba na 
90% ya waliopo kwenye tiba wawe na kiwango kidogo cha  Virusi kwenye damu


Katika ziara hiyo Konga za Halmashauri ya Igunga na Biharamuro walikuwa wageni walioitembelea konga ya Muleba. Konga hizo ziliwakilishwa na Wenyeviti wa Konga, Waratibu wa kudhibiti UKIMWI Halmashauri (CHAC ), Mwenyekiti wa kamati ya kuzibiti UKIMWI Halmashauri (CMAC), Mwenyekiti wa kamati za kudhibiti UKIMWI ngazi ya kata (WMAC) na viongozi wawili wa Vikundi wezeshi.
 

Wageni hao toka Igunga na Biharamuro walitembelea na kuona miradi mbalimbali inayotekelezwa na vikundi vya wezeshi vya WAVIU vya Tumaini kutoka Kishanda, Imani kutoka Bunganhuzi na Njuna ya June kutoka Mushabago, 
Wanakikundi wa kikundi cha Imani wakionesha moja ya miradi yao ya ufugaji wa mbuzi
pia walitembelea Vituo vya Tiba na matunzo (CTC - Care and Treatment Center) vilivyopo Buganguzi na kituo cha Afya cha Rushwa.

Wageni wakipata maelezo kutoka kwa Mganga mfawidhi wa kituo cha Afya Buganguzi
Viongozi wa  Biharamuro, Igunga  na Muleba walipendezewa na ziara hiyo ya mafunzo na kubadilishana uzoefu  na kupendekeza kufanyika mara kwa mara. Pia walitoa uzoefu wao kama mapendekezo kwa konga ya Muleba na Vikundi Wezeshi vya Konga hiyo.
 
Pamoja na mapendekezo hayo waliyoyatoa waliwashukuru na kuwasifu Konga na Vikundi Wezeshi vya WAVIU wa Muleba kwa vitu vifuatavyo:-

         Kuratibu na Kusaidia Vikundi vya Wezeshi vinavyoundwa na halmashauri ya Muleba
·        Huduma za ART zinazotolewa katika ngazi ya kituo
Huduma, Ushirikiano na utetezi kwa WAVIU unaotolewa katika zahanati/CTC ya Rushwa na Buganguzi
         WAVIU wengi wa Konga Muleba Virusi vyao vimefubaa kitu kinachowawezesha kujikita zaidi kwenye shughuli za maendeleo ya kiuchumi na Kijamii 
         Msaada unaotolewa na vikundi vya Wezeshi  katika kuwalea watoto yatima  wanaoishi na VVU na wasiokuwa na VVU

Watoto wanaolelewa na kusomeshwa na wanakikundi wa kikundi cha Imani baada ya wazazi wao kufariki
Tushebe Matunda ni mtoto wa miaka minne (4) anaelelewa na wanakikundi wa Tumaini Kishanga baada ya Mzazi wake kufariki siku sita kabla ya kujifungua

Baada ya ziara hii kulifanyika kikao cha majumuisho kwa konga zilizoshiriki Igunga, Muleba na Biharamulo kwa kuangalia nini wamejifunza ,nini wanashauri kifanyiwe kazi na kukubaliana ni kipi wanakwenda kufanyia kazi ambapo moja ya ahadi zilizotolewa ilikuwa
ya mwenyekiti wa Halmashauri ya Igunga bwana Lucas Bugota aliyeahidi kuwa " mimi pamoja na viongizi wa Konga tuliokuja kujifunza tukitoka hapa tutaenda kuandaa mpango kazi kwa ajili ya utekelezaji wa yale yote tuliojifunza tunaomba baada ya miezi mitatu mje igunga kwa ajili ya kuona shughuli zetu  tulizozifanyia maboresho na kujifunza pia"


Mnamo 7 Februari 2019,  NACOPHA ilitoa mrejesho/ mapendekezo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Muleba, aliyefurahia na kupendezwa na kazi kubwa inayofanywa na  Konga ya WAVIU wa Halmashauri ya Wilaya ya Muleba.

Kikao cha mrejesho wa ziara na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Muleba Mhe. Emanuel Sherembi
Mapendekezo yaliyotolewa ni pamoja na Halmashauri zione jinsi gani zitawatumia WAVIU/ Wakili tiba kusaidia kutoa huduma ambazo sio za kitabibu katika vituo vya afya ili kupunguza adha ya upatikanaji wa huduma katika vituo vya tiba na matunzo, Mashirika yanayofanya miradi ya afua za UKIMWI kutumia mfumo rasmi wa konga kufanya kazi na WAVIU tofauti na ilivyo sasa wanawatumia WAVIU bila kupita Konga ,Viongozi wa dini wapewe mafunzo juu ya masuala ya VVU/UKIMWI kwa sababu wengi wao wamekuwa wakiwashawishi WAVIU waache dawa mara baada ya kuombewa. 





Makamu Mwenyekiti Halmashauri ya Biharamuro akikabidhi kiasi cha Shilingi elfu themanini na sita za Kitanzania kwa Mlezi wa Tushebe Matunda baada ya wajumbe waliotembelea kikundi hicho kuguswa na namna kikundi kilivyojitolea kumlea mtoto 






WANAUME IRINGA WAAMSHWA TENA VVU


Na Friday Simbaya, IRINGA
Mkuu wa Wilaya ya Iringa Richard Kasesela, amewataka wanaume kujitokeza kwa wingi kupima VVU ili kujua hali zao na kama wakugundulika waanze dawa mara moja.
Alisema kuwa utafiti unaonesha kwamba wanaume wako nyuma katika masuala ya kupima VVU ukilinganisha na wanawake.
Kasesela alisema hayo wiki iliyopita wakati wa uzinduzi wa filamu itwayo ‘PILI’ ya masuala ya VVU na UKIMWI katika Mkoa wa Iringa katika viwanja vya Mwembetogwa, iliyoanza kuonekana kuanzia saa moja 1 jioni hadi saa tatu usiku.
Alisema kuwa Iringa inakabiliwa na changamoto ya masuala ya UKIMWI kwa vile inashika nafasi ya pili katika maambukizi ya VVU baada ya Mkoa wa Njombe anaoshika nafasi ya kwanza kitaifa.
Kasesela alieleza kuwa  kuna faida ya kupima VVU na hatimaye kujua hali yako kwa vile Serikali inatoa ARVs za kupunguza makali ya VVU bure kupitia Msaada wa Mfuko wa dharura wa Raisi wa Marekani wa kupambana na UKIMWI (PEPFAR).
“Kupima VVU na kujua hali zetu za afya hasa kwa wanaume kutapunguza kasi ya maambukizi ya VVU mkoani Iringa, hivyo naomba wanaume wenzangu tuwe mstari wa mbele” Alihimiza DC Kasesela.

Pia alilipongeza Baraza la Taifa la Watu Wanaishi na VVU (NACOPHA) kwa kushirikiana na Ubalozi wa Marekani kwa onesho la filamu ya “PILI”.
Inalenga kuwafikishia ujumbe vijanakukiwa ni mwendelezo wa maadhimisho ya miaka 15 ya msaada wa PEPFAR katika kuwezesha wanaoishi na VVU (WAVIU) hasa vijana.
 Mratibu wa uzinduzi wa filamu ya “PILI” kutoka NACOPHA bwana Edward Uisso alisema lengo kuu la onesho la filamu/sinema hii ni ukuza ongezeko na ufikiwaji wa huduma za VVU hususani kwenye tiba na matunzo miongoni mwa vijana wadogo wanaoishi na VVU kupitia kutambua mchango na msaada wa PEPFAR katika mwitikio wa kitaifa wa UKIMWI kwa kutumia WAVIU kama wanufaikaji wa msaada kutoka PEPFAR nchini Tanzania.

Aliongeza kuwa malengo mengine ni kushirikisha jamii katika ongezeko la ufikiwaji na utumiaji wa huduma za VVU hasa kwenye tiba na matunzo na kutumia filamu hii kama zana ya uwezeshi  kwa vijana wadogo wanaoishi na VVU katika kutatua na kupambana dhidi ya unyanyapaa na ubaguzi.
Uisso aliongeza kuwa unyanyapaa binafsi kwa WAVIU bado ni changamoto kubwa ukiachilia mbali unyanyapaa utokanao na tamaduni na imani za kidini.
Alisema ushirikishwaji wa jamii ni ufunguo katika kuelimisha jamii juu ya madhara ya unyanyapaa kwa WAVIU na katika kufikia sifuri ya unyanyapaa ifikapo mwaka 2030.
“Uzinduzi huu wa filamu ya PILI ni wa tano kimkoa,  kwani kwa mara ya kwanza filamu hii ilizinduliwa kwa mkoa wa DSM tarehe 8/11/2018, Mwanza tarehe 23/11/2018, Mbeya tarehe 30/11/2018, Njombe ni leo tarehe 7/12/2018 na kilele kitakuwa kwa Mkoa wa Iringa tarehe 14/12/2018 ikiwa ni kubadilishana uzoefu kwa watu wanaoishi na VVU kama wanufaikiaji wa msaada wa PEPFAR nchini”. Alisema Uisso.



PILI anaishi  kijijini nchini Tanzania, akifanya kazi ya kibarura shambani akilipwa ujira wa chini ya dola mbili (Sh 2,600) kwa siku ili aweze kupata chakula kwa watoto wake wawili
Anaishi anahangahika kukabiliana na hali yake ya kuwa na VVU kwa kificho.